Katika kuendeleza jitihada za kuimarisha utalii wa chakula barani Afrika, leo Aprili 23, 2025, Jiji la Arusha limekuwa mwenyeji wa Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Utalii wa Vyakula Afrika. Mkutano huo umefanyika katika Hoteli ya Gran Meliá, huku ukijumuisha wadau mbalimbali wa sekta ya chakula na utalii kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika.
Mgeni rasmi katika mkutano huo ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, ambaye amepongeza juhudi za Umoja wa Mataifa katika kukuza utalii wa vyakula, akieleza kuwa sekta hiyo ni nyenzo muhimu ya kuinua uchumi wa nchi nyingi za Afrika.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mheshimiwa Paul Christian Makonda, ameuelezea mkutano huo kama fursa adhimu kwa Arusha na Tanzania kwa ujumla, kutangaza utajiri wa vyakula vya asili, utamaduni na vivutio vya kipekee vya utalii vilivyopo nchini.
“Kupitia mkutano huu tunapeleka ujumbe kwamba Tanzania haijajaliwa tu vivutio vya asili, bali pia utamaduni wa chakula unaoweza kuwa kivutio kikubwa cha watalii duniani. Arusha iko tayari kuwa kitovu cha utalii wa vyakula Afrika.”
Tanzania inaendelea kujiweka kama kinara katika sekta ya utalii barani Afrika, huku Arusha ikiimarika kama lango kuu la Sekta ya Utalii.
Hatimiliki ©2018 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Arusha. Haki Zote Zimehifadhiwa