Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Paul Christian Makonda, leo tarehe 03 April, 2025 ameshuhudia utiaji saini wa mkataba kati ya uongozi wa halmashauri ya Jiji na wakandarasi kwaajili ya ujenzi wa mradi wa barabara ya Eso - Longdon yenye urefu wa kilometa 1.8 kwa kiwango cha lami inayounganisha kata ya Ungalimited na Sokoni I pamoja na ujenzi wa Ukumbi wa kisasa wa mikutano wa Halmashauri Jiji la Arusha.
Katika hafla hiyo iliyofanyika Kata ya Ungalimited, Mhe. Makonda amewataka wakandarasi hao kutekeleza miradi hiyo kwa viwango vilivyokubaliwa na kumaliza miradi kulingana na mikataba na kusisitiza wananchi wa maeneo hayo kutoa ushirikiano kadri itavyohitajika.
" Mkandarasi ambaye hataendana na kasi ya mradi tutamtoa kwake anapokaa na kumuhamishia kituo cha polisi awe anatokea hapo kuja kutekeleza mradi". Amesema Mhe. Makonda.
Mradi huo wa ujenzi wa barabara utatekelezwa kwa gharama ya shilingi bilioni 3.2 pamoja na ukumbi wa kisasa kwa gharama ya shilingi bilioni 6.2, fedha za mapato ya ndani ya halmashauri hiyo.
Hatimiliki ©2018 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Arusha. Haki Zote Zimehifadhiwa