Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe.Paul Christian Makonda amesisitiza umuhimu wa wananchi wa Mkoa wa Arusha kudumisha na kutunza amani na utulivu mkoani hapa, akiwataka kufuata taratibu pale panapotokea migogoro ama sintofahamu za kiutendaji kwenye maeneo yao.
Akizungumza na wananchi wa Mtaa wa Longdon- Mazengo Kata ya Sokoni One leo Jumanne Aprili 15, 2025, Mhe. Makonda pia amewahimiza kuwa na utamaduni wa kuhudhuria vikao kati yao na Viongozi wa maeneo yao, ili kujua mipango ya Maendeleo katika maeneo yao sambamba na kuwasilisha kwa viongozi wao changamoto mbalimbali zinazowakumba.
"Linapotokea jambo fuateni utaratibu wa kuwafuata viongozi wa serikali sambamba na kushiriki kwenye vikao vyote vya msingi ili kusikiliza na kutoa maoni kuhusu maendeleo katika maeneo yenu badala ya kuandamana na kujitangaza hali inayoweza kuleta taharuki na kuchafua taswira ya Mkoa wetu.Mkitumia utaratibu unaofahamika na taarifa zikanifikia nitashughulika na kila mmoja anayehusika kukwamisha shughuli za maendeleo." Amesema Mhe. Makonda.
Mhe. Makonda amefanya ziara hiyo leo mahususi kwaajili ya kuwasikiliza wananchi hao ambao wamekuwa wakilalamika kuhusu kivuko kichopo katika mtaa huo akiahidi kuwa serikali inaendelea na jitihada mbalimbali za kuhakikisha kuwa miundombinu ya Mkoa wa Arusha inakuwa sawa na yenye kupitika kwa nyakati zote.
Hatimiliki ©2018 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Arusha. Haki Zote Zimehifadhiwa