Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Paul Christian Makonda leo Jumatatu Februari 17, 2025 amekutana na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) akihimiza suala la Ujenzi wa viwanda na ufufuaji wa Viwanda vilivyokufa Mkoani Arusha kama sehemu ya Mkakati wa kukuza dhamira njema ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kukuza fursa za ajira kwa Vijana wa Tanzania.
Mbele ya Wajumbe wa Kamati hiyo, Mhe. Makonda amesisitiza umuhimu wa kuinganisha sekta ya Utalii na sekta ya Viwanda, akisema kuwa Ujio wa wageni mbalimbali Mkoani Arusha ni fursa kwa wawekezaji mbalimbali kujenga Viwanda kwani mahitaji ya bidhaa mbalimbali ni makubwa kuanzia kwenye nyumba za kulala wageni na sehemu nyinginezo.
"Kuanzia mgeni anapotua kwenye uwanja wa ndege mpaka anaporudi kwenye uwanja wa ndege humu ndani kuna viwanda vingi sana, kuna kiwanda cha sukari watu watatengeneza chai, Kuna viwanda vya mafuta ndiyo ndiyo maana watu wanapika, yaani ukivihesabu vile viwanda unakuta mpaka samani, magodoro nakadhalika." Amesema Mhe. Makonda.
Akikumbushia makubaliano yao ya kukutana na Waziri wa Viwanda Mhe. Seleman Jafo hivi karibuni kujadili kuhusu mustakabali wa sekta ya viwanda vya Arusha, Mhe. Makonda amesisitiza umuhimu wa bidhaa zote za hotelini ikiwemo mashuka na taulo kutengenezewa Mkoani Arusha ili kusaidia ongezeko la uzalishaji wa fursa za ajira kwa Vijana wa Arusha.
Copyright ©2017 Arusha Regional Comissioner's Office. All rights reserved.